Saturday, October 31, 2009

Chiligati Watanzania siyo mabwege!

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, John Chiligati amesema kitendo cha Rais Jakaya Kikwete, kutoa ardhi kwa wawekezaji si kuiuza nchi badala yake ni kukuza uchumi kupitia kilimo.

Chiligati amesema kuwa kitendo hicho hakiwezi kuwa ni kuuza nchi, kwa sababu wawekezaji wanakodishwa mashamba na wala hawamilikishwi, hivyo wakiondoka hawaondoki nayo.

Si kweli hata kidogo na ninadhani Bwana Chiligati anajua hiyo ni danganya toto. Mimi naona Chiligati, ambaye ni mkuu wa propaganda wa CCM anacheza na msamiati.

Kukodishwa maelfu ya ardhi ya Tanzania kwa miaka 99 ni nini, kama siyo kuuza? Ikipita miaka hiyo, huo mkodisho utaendelea – kwa miaka mingine 99. Ni nini hiyo? Na WaTanzania ambao watakuwa vitukuu na vilembwe wa watawala wa leo, na ambao wengi wanaishi vijijini, wataenda wapi? Sidhani kama wote watakuwa mawaziri wa ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi au marais.

Kwa mtu yeyote anayeifikiria na kuipenda nchi yetu, atagundua kuwa huu ni ubinafsi mbaya sana. Kwa nini tunafikiria kama kuku? Maana yake kuku anaangalia njaa yake pale pale.Akishiba basi umetoka hiyo. Kesho itajijua yenyewe.

Wakati wa uhuru, miaka arobaini na iliyopita, Tanganyika ilikuwa na wananchi 12 milioni. Leo tupo 45 milioni. Wamezidi watu 30 na, milioni. Tukianza kuuza ardhi (mimi naona ni uhaini tu) na baada ta miaka 99 utakuwa na watu 70 milioni. Je,utawaweka wapi? Nchi yetu itakuwa ni ya manamba tu? Na waTanzania hawatakubali hiyo – zitapigwa tu!

Ukiangalia historia kidogo watawala waliota, baada ya kuambiwa na wakoloni mambo-leo, kuwa bila Tanzania kubinafsisha viwanda vyetu hatuwezi kuendela. Tumebinafsisha, tena kwa bei chee, na sasa tumebaki tunang’aa macho.

Juisi za embe na mananasi ‘zinatengenezwa’ nchini Saudi Arabia. Watanzania hawawezi kusindika juisi hizo. Nguo nzuri za pamba inayolimwa Shinyanga ‘zinatengenezwa’ Dubai. Watanzania hawawezi kushona nguo za pamba. Matusi hayo kwa Tanzania Bwana Chiligati! Inaonekana kuwa Watanzania hatuwezi kufanya lo lote.

Sasa anasema, na hiyo ni sauti ya watawala wetu, kuwa nchi yetu bila kuwa na wawekezaji katika kilimo cha mashamba makubwa haiwezi kuendelea. Huu utumbo tutaendelea kusikia mpaka lini? Hizi fikira tegemezi za watawala wetu zitaendedea mpaka lini?

Kujidharau gani huko kwa watawala, na kudharau waTanzania wenzao kuwa hawawezi kulima mpunga na ngano. Mpunga ni mpunga na ngano ni ngano. Kuna watumwa wa kimawazo (inferiority complex) ambao wanafikiria kuwa waarabu au wakorea wakilima mpunga unakuwa mzuri kuliko ule unaolimwa na mmatumbi huko Ifakara. Mtu mweupe akisema, hata upumbavu gani, anasikilizwa sana na watumwa hao wanaowahusudu watu weupe.

Haya tusaidiane – tunapata maendeleo gani kutoa ardhi yetu kwa wakoloni ambao watawala wanawaita wawekezaji. Tunapata nini kutoka kwenye kashfa ya Loliondo. Eti shule moja na kiwanja cha ndege. Ni lini wamasai wa Loliondo waliiambia serikali kuwa wanataka kiwanja cha ndege?
Tuambiwe faida tanayoipata au tutakayo ipata kwa kinadi ardhi yetu. Jamani kama hamna la kufanya, basi kuleni maraha tu. Lakini ardhi yetu muiache. Kama mtu hana la kufanya basi akae anywe chai. Siyo lazima aanze kuota cha kufanya. Ardhi yetu muiache!

1 comment:

Anonymous said...

Kuna msemo unaosema mjinga pa kwenda na si pakurudi.Kwani tumeyaona haya kutoka Southern Rhodesia[wakati wa John cecil Rhodes na kina Monumutapa]shanga kwa aridhi.Biashara hiyo imepitwa na wakati.Kitendo hiki kitapigiwa kelele na umma na hatimaye hata wajukuu watakuja kusema kinababu walituuza,je utapata utulivu kaburini?.