Friday, June 12, 2009

CHOMBEZO LA ADAM LUSEKELO

CCM sasa wataka ukomo wa uongozi?

Nasikia yanatoka Mwanza hayo, CCM sasa wameanza kugundua kuwa kwa kweli demokrasia ya kweli ni ndoto tu. Hapa tunazungumzia katika ‘demokrasia’ yetu ya kinamna tu. Haina itikadi, msimamo wala nini – ni pochi yako tu. Hamna kitu kipya kinasemwa. Kila chama kinazungumzia ‘maendeleo’ na kupambana na rushwa. Ambayo tunajua ni masihara tu.

Kwanza wabunge wenyewe wa CCM walichoshwa na vibano kutoka kwa wakubwa wao wa chama. Eti wabunge wa CCM wanakaa kama kamati. Hamna hiyo! Wanaenda kupata kibano iliwaseme wanachoambiwa – siyo wanavyofikiria. Kwa lugha ya kawaida tunaita udicteta katika chama.

Sasa dogodogo wa chama wanasema kuwa kama mambo yatakuwa yanaendela hivi basi kamwe hawatakuwa na chansa ya kuwa viongozi wa chama hicho. Ni kwamba kuna mizee ambayo haitaki kung’atuka katika uongozi wa chama hicho.

Sasa wanasema kuwa endapo katiba ya chama hicho itaweka ukomo wa uongozi kwa wanachama kama ilivyo sasa kwa urais ndani ya katiba ya nchi itasaidia kutokomeza vitendo vya rushwa ndani ya chama – na tumeona laivu, yaani.

Na kwa nini rais tu? Kila mtu lazima aambae, lazima ang’atuke. Mawaziri, makatibu wakuu, ma-lejino kamishna, kila mtu. Pia huwezi kuwa mjumbe wa Halmashauri Kuu kuanzia UHURU hadi leo. Kwani we ni nani bwana?

Huwezi mtu kuwa waziri kuanzia Adam na Hawa. Huko ni kujifanya huoni sheria za Mwenyezi Mungu. Huwezi mtu ukawa bosi katika awamu zote nne. Huko ni kwa upande wa watawala kuwatukana Watanzania.

Mmoja wa dododogo wa CCM huko Mwanza, Lucas Mashilanga ameshauri kiwango cha miaka kumi kinatosha. Bwana Mashilanga angeelewa kitu kimoja. Sisi binadamu kimsingi ni waroho.

Mpe mtu yo yote ulaji basi atataka akae hapo hapo mpaka siku atakayokwenda kwa muumba wake. Na kama itawezekana ampasie mtoto , au hata mjukuu wake nao waendelee na ulaji. Kila mtu chini ya ngozi yake anapenda kuwa mfalme.

Sasa naona Bwana Mashilanga amekuwa anawasikiliza viongozi wake waki-rap sana kuhusu demokrasia. Naona alianza kuamini na ku-rap utumbo huo kuhusu demokrasia. Kitu ambacho amesahau ni kuwa demokrasia inaonyeshwa kwa vitendo, siyo blah…blahhh.

Pia ndugu yangu na ndugu zangu wengi wamekuwa wakiota kuwa wananchi wanapewa demokrasia na viongozi. Hamna hiyo! Demokrasia inapiganiwa. Uhuru siyo kitu cha bure ambacho kinatolewa kama zawadi kutoka kwa watawala. Vitu hivyo vinapiganiwa kutoka katika kila kona ya jamii. Ukikaa kimya nao watakaa kimya na kutawala mpaka wakienda makaburini mwao.

No comments: